Chanzo cha Majipu Matakoni na Tiba

majipu matakoni
jipu matakoni

Majipu matakoni ni hali ya kufanyika kwa kinundu kilichojaa usaha kwenye eneo la matako karibu na mkundu. Jipu huleta maumivu makali sana, homa, kutokwa na uchafu na kukosa nguvu kwa mgonjwa.

Majipu ya matakoni mengi hutokea kutokana na maambukizi kwenye tezi za kwenye eneo la mkundu. Kwa baadhi ya wagonjwa, majipu haya yanaweza kupelekea fistula la mkundu. Ampapo jipu linachelewa kupona mpaka kupelekea kupasuka kwa ngozi karibu na eneo la haja kubwa.

Nini kinasababisha majipu matakoni?

Kuziba kwa tezi za eneo la haja kubwa, magonjwa ya zinaa ama maambukizi kwenye tezi za mkundu vinaweza kupelekea majipu haya. Vitu vingine hatarishi vinavyopelekea majipu matakoni ni pamoja na

  • kuugua magonjwa ya mgumo wa chakula kama ulcerative colitis na Crohns disease ambapo yanapelekea kinga ya mwili kushambulia seli za mwili mara kwa mara.
  • kisukari
  • kuvurugika kwa kinga ya mwili kutokana na kuugua ukimwi
  • ngono kinyume na maumbile
  • matumizi ya baadhi ya dawa kama prednisone
  • mgonjwa aliyepo kwenye tiba ya chemotherapy
  • kukosa choo na kupata choo kigumu na
  • kuharisha

Watoto wenye historia ya kupasuka njia ya haja kubwa, wapo kwenye hatari kubwa ya kuugua majipu matakoni. Kupasuka kwa njia ya haja kubwa hutokea sana kwa watoto wenye kupata choo kigumu na kukosa choo kwa muda mrefu.

Dalili za majipu matakoni

Maumivu ya mara kwa mara kwenye eneo la haja ubwa ni moja ya sababu kubwa kwamba una jipu. Maumivu haya huambatana na kuvimba na pia maumivu makali wakati wa kujisaidia.

Dalili zingine za jipu matakoni ni pamoja na

  • kupata choo kigumu
  • kutokwa na uchafu mkunduni
  • kuvimba kwa ngozi karibu na eneo la haja kubwa na
  • kuishiwa nguvu

Baadhi ya wagonjwa hupata nundu yenye rangi nyekundu iliyozimba na laini eneo la mkundu. Mgonjwa pia anaweza kupata homa kutokana na maambukizi aliyonayo. Unaweza pia kutokwa damu mkunduni au kushindwa kukojoa vizuri.

Jipu linaweza kujitokeza ndani kabisa ya eneo la haja kubwa, na kusababisha maumivu makali ya tumbo.

Vipimo kugundua uwepo wa majipu matakoni

Daktari anaweza kugundua uwepo wa jipu matakoni kwa kukutazama kwa macho kuona mahali penye uvimbe karibu na eneo la haja kubwa.

Katika baadhi ya wagonjwa, jipu linaweza lisionekane kwa macho katika eneo la mkundu. Daktari atahitaji kutumia kifaa cha endoscope kutazama eneo la ndani ya mkundu.

Endapo jipu litakuwa ndani zaidi, daktari anaweza kupendekeza ufanyiwe kipimo kikubwa cha MRI au utrasound kupata picha zaidi ya tatizo lako.

Matibabu ya majipu matakoni

Majipu ya matakoni kwa baadhi huisha yenyewe bila kuhitaji tiba. Tiba moja ya haraka na rahisi, ni kwa daktari kupasua jipu na kuminya uchafu wote. Baada ya hapo utasafishwa na kuwekewa dawa .

Kama jipu la matakoni halitatibiwa,linaweza kubadilika na kuleta fistula. Fistula ni pale kinyesi kinaoanza kutoka kwenye eneo la jipu.

Baada ya upasuaji mdogo kuondoa jipu, inashauriwa kuoga maji ya vuguvugu. Kukaa kwenye beseni lenye maji ya uvuguvugu inasaidia kutoa uchafu wote kwenye jipu na kupunguza uvimbe.

Daktari pia anaweza kukupatia antibiotics kutibu maambukizi ya bakteria.

Jinsi gani ujikinge kupata majipu matakoni?

Baadhi ya hatua za kuchukua ni pamoja na

  1. Kujikinga dhidi ya magonjwa ya zinaa na kupata tiba mapema endapo utaugua
  2. Epuka kabisa kufanya tendo kinyume na maumbile
  3. Kusafisha eneo la haja kubwa ni muhimu kwa watu wazima na watoto.

Ukiwa na maswali wasiliana nasi kupitia whatsapp namba 0678626254.

Bofya kusoma kuhusu: Kuvuja shahawa (semen leakage)wakati haupo kwenye tendo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *