Choo Chenye Kamasi

Kwenye makala yote ukiona neno kamasi, haina maana ya makamasi ya pua, ni ute mzito unaozalishwa maeneo mbali mbali ya mwili. Mwili unatengeneza uteute mzito ili kusaidia kulinda na kulainisha vungo vya mwili. Ndani ya utumbo na tumbo pia kuna uteuute.

Uteute au kamasi hili ni kinga

Pia kazi ya ute ama kamasi hilo ni kuzuia athari ya vimelea wabaya kama bakteria, virusi au fungus. Ute huu pia unalinda tumbo dhidi ya tindikali na vimiminika hatarishi.

Ukiwa na afya njema, waweza kupata choo kinachoambatana na kamasi kwa kiwango kidogo. Hili siyo tatizo mpaka kuwe na viashiria vingine ambavyo nitaeleza hapa chini.

Endelea kusoma zaidi kujua chanzo cha tatizo, nini cha kufanya kuepusha tatizo na muda gani umwone daktari.

Chanzo cha kamasi kwenye haja kubwa

1.Maambukizi kwenye utumbo

Maambuki haya yanaweza kuwa ya bakteria au fungus yanapelekea upate choo chenye kamasi. Tafiti zinasema kwamba bakteria wanachochea uzalishaji wa ute kwenye utumbo na hivo kupelekea choo chenye kamasi.

2.Utumbo kushindwa kufyonza chakula(malabsorption)

Ufyonzaji wa chakula unafanyika kwenye utumbo mdogo. Viini lishe hufyonzwa na mabaki hutolewa nje kama kinyesi. Endapo chakula hakijafyonzwa vizuri, waweza kupata choo chenye makamasi.

3.Fistula ya mkunduni au vidonda vya kwenye mkundu

Fistula ya eneo la mkundu, inatokea pale ngozi ya nje pembeni ya haja kubwa inapotengeneza shimo kuelekea ndani. Shimo hili laweza kuvujisha choo na uteute pia. Vidonda vya ndani ya haja kubwa pia hupelekea upate choo chenye makamasi

4.Saratani ya utumbo mpana ama saratani ya eneo la mkundu

Saratani eneo la utumbo na haja kubwa zaweza kupelekea upate choo chenye damu pamoja na kamasi. Usipate hofu kwamba tayari una saratani kila unapopata choo chenye makasi. Tazama na dalili zingine

Dalili zingine za saratani ya utumbo ni

  • Maumivu ya tumbo , tumbo kujaa gesi na mwili kutokuwa na usawa.
  • Mabadiliko kwenye choo kama kuharisha na kupata choo kigumu ama kukosa choo kwa muda mrefu, dalili hizi zinaweza kuwa za muda mrefu
  • kupata choo chenye damu ama choo cheusi na chenye nta
  • mwili kuchoka sana
  • kicheuchefu na kutapika
  • kukosa hamu ya kula na mwili kupungua uzito kwa kasi
  • mwili kuishiwa damu (anemia)
  • macho na Ngozi kuwa ya manjano (jaundice)

Vipimo kuhusu tatizo la choo chenye kamasi

Kwenye changamoto ya kupata choo chenye makamasi, hakuna kipimo kimoja tu cha kujua chanzo cha tatizo, ni vipimo vingi.

Daktari atakusikiliza kwa umakini kuhusu dalili unazopata na kuanza kwa kipimo cha damu ili kuona kama kuna maambukizi.

Baada ya hapo daktari anaweza kupendekeza vipimo zaidi. na vipimo vinahusisha

  • sampuli ya choo
  • colonoscopy-kugundua uwepo wa saratani
  • X-ray ili kuona viungo vya ndani
  • MRI ili kuona kwa kina zaidi kuhsu tishu na viungo
  • CT scan ya tishu na utumbo

Matibabu ya tatizo la choo chenye kamasi

Kwasababu tatizo la kamasi linaweza kuashiria dalili ya changamoto nyingi, tiba inategemea na chanzo cha tatizo lako.

Kwa kesi za kawaida ambapo chanzo cha tatizo ni kukoa choo ama kupata choo kigumu au kuishiwa maji, hapo unaweza kubadili tu mambo machache, ukatibu tatizo.

Fanya mabadiliko haya

  • ongeza kiwango cha maji unachokunywa
  • tumia zaidi vyakula vyenye kambakamba kwa wingi, ambavyo havijakobolewa

Daktari atakuandikia dawa kila baada ya kipindi fulani, endapo una matatizo sugu yanayopelekea upate choo cha kamasi.

Kama daktari atagundua una saratani, atakupa rufaa ya kwenda kwa daktari bingwa wa saratani. Hapo utaanzishiwa dawa na mionzi.

Bofya kusoma zaidi kuhusu: Choo kigumu na tiba bila kumeza vidonge